VYAMA VYA SIASA VYATAKIWA KUJIENDESHA KAMA TAASISI IMARA

Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Mhe. Jaji Francis S.K Mutungi, amevitaka vyama vya siasa kudumisha na kuimarisha demokrasia ndani ya vyama vyao ili viweze kutekeleza majukumu yao kama taasisi imara.
Amesema endapo vitafanya hivyo vitapingana na mawazo ya walio wengi kuwa vyama wanavifananisha na Vikundi ya Kuweka na Kukopa (SACCOS)
Wito huo ameutoa leo Septemba 19 , alipokuwa anafungua mkutano wa siku mbili na Viongozi wa Kitaifa wa vyama vya siasa kwa ajili ya kuvijengea vyama hivyo uwezo wa masuala ya rasilimali fedha na rejista ya chama ili viweze kujiendesha kama taasisi uliofanyika katika ukumbi wa Ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es salaam.
Jaji Mtungi alisema ni muhimu kujenga vyama kama taasisi imara kwani mtu yeyote kutoka nje anayehitaji kuwekeza katika vyama hawezi kufanya hivyo ikiwa chama kina hati chafu kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
‘’Mafunzo ya rasimali fedha na regista ya vyama kama vile mali za vyama ni muhimu kwa sababu pamoja na kupatiwa mafunzo haya ni vyema mkatambua kuwa vinawajibika kwa wananchi katika suala zima la utendaji wa ndiyo maana msajili analazimika kufanya ukaguzi katika vyama,”alisema.
Pia, aliwaambia wawakilishi wa vyama vya siasa kuwa elimu ya fedha na regista ya chama ni muhimu kwa sababu inasaidia sana kupunguza migogoro ndani ya vyama vya siasa.
Alisema semina kama hizo zinazotolewa na ofisi ya msajili zinapunguza migogoro ndani ya vyama vya siasa kutokana na migogoro mingi kuwa ni ya fedha na mali za chama.
Vilevile, alivitaka vyama hivyo kushindana katika weledi na hoja zinazokubalika kwa umma ili viweze kuvuna wanachama wengi kuliko kukaa na kuanza kutupiana lawama zisizokuwa na msingi.
Naye, Makamu Mkuu Mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Rwekaza Mkandala ambaye aliwasilisha mada ya jinsi ya kuendesha chama kama taasisi, alisema lengo la chama cha siasa chochote ni kujiandaa kushika madaraka au kuwa wapinzani wa serikali hivyo lazima kuhakikisha vinajijenga kama taasisi inayoaminika kwa wananchi.
Profesa Mkandala alisema vyama vingi hapa nchini ni matokeo ya ukoloni mamboleo ambao ulianza kushamiri mwaka 1990 ambapo Tanzania kama zilivyo nchi nyingine Barani Afrika zilikumbwa na mabadiliko ya kiuchumi ya soko huria ikiwemo nchi zilizokuwa za ujamaa kuanza kufuata masharti ya Shirika la Fedha Duniani IMF.
Alisema ili chama kitambulike na kukubalika kama taasisi inabidi kutimiza au kuwa na vigezo muhimu ambavyo ni itikadi, uongozi bora, wanachama, muundo, demokrasia...